Wednesday, May 30, 2012

Dk. Slaa aitangazia vita CUF


KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willbroad Slaa, amesema harakati za kuendesha mchakato mzima wa ‘Vua gamba, Vaa gwanda’ ni lazima zikiguse pia Chama cha Wananchi (CUF) kwa vile kimeungana na CCM na kushindwa kutetea masilahi ya wananchi hususan wakazi wa mikoa ya Mtwara na Lindi.
Akihutubia mkutano wa hadhara katika Kata ya Mkanaledi mkoani Mtwara jana, Dk. Slaa alisema tokea kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, Chama cha CUF kilipata uungwaji mkono kwa kiasi kikubwa na wakazi wa kusini hivyo kushindwa kutetea masilahi yao na kuungana na CCM ni sawa na kuwaambia wananchi wajitafutie ukombozi mwingine.
“CUF tulikubaliana nao, kwakuwa wote ni wapinzani na wao wana nguvu huku na maeneo ya pwani ni vema tukawaachia ili waendeleze jukumu la kuwakomboa Watanzania,” alisema Dk. Slaa na kuongeza:
“Ndio sababu hatujawahi kuweka mgombea urais katika uchaguzi wowote kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, lakini kitendo cha CUF kuungana na CCM kimeonyesha dhahiri hawana nia ya kuwakomboa Watanzania,” alisema.
Dk. Slaa alisema wakati wa wakazi wa Mtwara, Lindi na maeneo mengine kuendelea kunung’unika umepita na kinachotakiwa ni kuchukua maamuzi magumu kwa kuikataa CCM na kujiunga na CHADEMA.
Akizungumzia rasilimali za mikoa ya kusini, Dk. Slaa alisema mikoa ya Lindi na Mtwara inaongoza kwa kuzalisha zao la mihogo na korosho na kama mazao hayo yangetumika vema yangesaidia kuleta maendeleo.
“Ninyi mna rasilimali za kutosha sasa kama gesi, mihogo na bandari hizi zikitumika ipasavyo hakuna kati yenu atakayelalamikia huduma mbovu za serikali lakini hamna kinachofanyika,” alisema Dk. Slaa.
Alisema serikali haikuwa na nia ya kweli ya kuwasaidia wananchi ndiyo maana ikaamua kuuza kiwanda cha kubangulia korosho kwa Mama Anna Mkapa kwa shilingi milioni 50 huku wananchi wakiendelea kutaabika.

0 comments:

Post a Comment